Dodoma FM

Serikali yaweka mifumo kuhakikisha inawatambua watumishi walio staafu na kuwalipa malimbikizo yaliyo salia

21 June 2021, 10:24 am

Na; Yussuph Hans.

Serikali imesema katika kuhakikisha watumishi waliostaafu wanapata mafao yao imetengeneza mifumo ya tehama kwa ajili ya kuwatambua wananchama wote pamoja na kulipa malimbikizo yaliyosalia.

Hayo yamebainishwa leo Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira Mh Patrobas Katambi wakati akijibu swali la Mbunge wa Kibaha Vijijini Mh Michael Constantino, aliyehoji Serikali ina mkakati gani wa kuisadia Wananchi waliostaafu wanapata mafao yao kwa wakati.

Mh katambi amesema kuwa serikali imetengeneza mifumo ya TEHAMA ya utambuzi wa wanachama hao, kulipa malimbikizi ya mafao na kuandaa ofisi kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma ya haraka Nchi nzima.

Aidha amesema kuwa wanaendelea kuwawajibisha viongozi wanaofanya uzembe katika ukusanyaji wa michango, huku baadhi ya kesi zikiwa zinaendelea mahakama mbalimbali Nchini.

Kwa upande mwengine Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Mh David Silinde amesema kuwa kupitia mradi wa serikali wa kuboresha shule za sekondari Nchini utachangia kutatua changamoto ya uhaba wa shule hizo.

bunge limeendelea leo Jijini Dodoma kujadili bajeti ya serikali ambapo ni mkutano wa tatu kikao cha hamsini na tano.