Dodoma FM

Immelezwa kuwa mila potofu katika jamii zinachangia watu kushindwa kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia

22 July 2021, 2:35 pm

Na; Shani Nicolous.

Imeelezwa kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vyombo vya usafiri hasa wa umma vimekithiri ingawa bado watu wana uelewa mdogo kuhusu ukatili huo.

Akizungumza na Dodoma Fm mkaguzi wa polisi dawati la jinsia Teresia Mdendemi amesema kuwa kuna ukatili mkubwa unafanyika hasa kwa wanawake hata lugha za matusi ni makosa ya jinai hivyo yeyote atakayefanyiwa vitendo hivyo asisite kuripoti katika vyombo vya sheria.

Amesema kuwa askari wa usalama barabarani wamekuwa wakiwapeleka wahanga wa vitendo vya ukatili katika dawati la jinsia hivyo ikitokea umefanyiwa ukatili huo popote utakapokuwa askari aliyekaribu na wewe apewe taarifa hizo bila kujali yupo katika kitengo gani kwa muda huo.

Ameongeza kuwa mila potofu zilizopo katika jamii ndiyo chanzo cha baadhi ya wahanga kutokutoa taarifa katika vituo vya sheria wakifanyiwa ukatili hivyo kama dawati la jinsia wanakemea mila potofu zinazochochea uonevu na ukatili kwa baadhi ya watu nchini.

Nao baadhi ya wananchi jijini Dodoma wamesema kuwa wamekuwa wakishuhudia vitendo hivyo katika usafiri wa uma lakini wanakosa elimu na nguvu ya kusema ukatili huo kwa vyombo vya sheria.

Ukatili wa kijinsi ni chanzo cha kupoteza nguvu kazi ya taifa,ongezeko la watoto wa mtaani, ongezeko la uhalifu, kutengeneza unyonge kwa muhanga hata kumsababishia madhara makubwa kisaikolojia.