Radio Fadhila

Mabalozi ‘Wamlilia’ Maalim Sief Sharif Hamad

19 February 2021, 9:56 AM

Mabalozi mbalimbali wanaowakilisha nchi zao hapa nchini, ‘wamemlilia’ Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad na kumuelezea kwa mema aliyoyafanya enzi za uhai wake hapa duniani.

Mabalozi hao wamewasili katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam kwa nyakati tofauti kwa ajili ya kusaini kitabu cha maombolezo ambapo mara baada ya kusaini kitabu cha maombolezo baadhi yao wakaelezea walivyoguswa na msiba wa Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad.

Balozi wa Ufaransa chini Tanzania, Mhe. Frederic Clavier amesema kuwa ni pengo kubwa kwa Zanziba na kwa Tanzania pia kwani Mhe. Maalim Seif alikuwa kiongozi mahiri kwa taifa na aliyekuwa na uhamasisho kwa bara la Afrika.

“Alikuwa mtetezi wa masuala mbalimbali ikiwemo demokrasia na haki, pia katika enzi za uhai wake alikubali kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais kwa Serikali ya Zanzibar ni jambo la kuigwa kwa taifa la Zanzibar na Taifa la Tanzania kwa Ujumla,” Amesema Mhe. Clavier

Mhe. Clavier ameongeza kuwa “Maalimu Seif alikuwa kiongozi aliyependa amani, na aliyekuwa mstari wa mbele kupigania maslahi ya nchi yake……lakini pia alikuwa mpenda amani na alikuwa mwanasiasa makini ……..kwa kweli tutamkumbuka daimia, tunamuombea kwa Mungu apumzike kwa amani,”.

Kwa upande wake Balozi wa Finland hapa nchini Mhe. Riitta Swan amesema kuwa Maalim Seif Sharif Hamad alikuwa kiongozi makini aliyependa amani na mshikamano wakati wa uhai wake.

“Kwa muda mfupi niliomfahamu kwa kweli alikuwa kiongozi mahiri aliyependa amani na umoja hakika pengo lake halitazibika kwa urahisi, Mungu ampumzishe kwa amani,” Amesema Mhe. Swan

Nae Balozi wa Zimbabwe hapa nchini, Mhe. ……amesema kuwa Mhe. Maalim Seif alikuwa ni kiongozi mchapakazi na mzalendo kwa taifa la Zanzibar na Tanzania. “Kwa kweli Jamhuri ya MUungano imepoteza kiongozi mzalendo, kwa niaba ya Jamhuri ya Zimbabwe natoa pole kwa Tanzania kwa kuondokewa na Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar…..poleni sana watanzania kwa msiba huu mzito,” Amesema Mhe.

Kwa upande wake Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Balozi Mubarak Mohammed Alsehaijan amesema kuwa Mhe. Maalim Sief kiongozi mpenda amani na atakumbukwa daima kwa mema aliyoyafanya kwa Wazanzibari na watanzania kwa ujumla.

Baadhi ya mabalozi waliofika na kusaini kitabu cha maombolezo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Jijini Dar es Salaam ni pamoja na Balozi wa Zambia nchini mhe. Benson Keith Chali, Balozi wa Finland chini Tanzania, Mhe. Riitta Swan na Balozi wa Kuwait nchini, Mhe. Balozi Mubarak Mohammed Alsehaijan.

Wengine ni Balozi wa Pakistani hapa nchini, Mhe. Mohammad Saleem, Balozi wa Ufaransa hapa chini, Mhe. Frederic Clavier, Balozi wa Zimbabwe hapa nchini, Mhe. Luteni Jenerali Mstaafu, Anselem Sanyatwe pamoja na Mwakilishi wa Balozi wa Irani hapa nchini. Bwn. Mohammad Rezaee.